Kikosi CECAFA: Aishi Manula, Juma Abdul Ndani Erasto Nyoni Nje Timu Ya Taifa

29th November 2019

DAR ES SALAAM, Tanzania- Kocha wa timu ya taifa ya Tanzania Bara, Kilimanjaro Stars, Etienne Ndayiragije amewataja wachezaji Juma Abdul wa Yanga mlinda lango wa Simba kwenye kikosi chake cha wachezaji 32

Aishi Manula
Aishi Manula
SUMMARY

Mechi ya mwisho kwa Manula kucheza akiwa na timu ya taifa ilikuwa ni mwezi Julai ambapo Stars walifungwa na Kenya kwa mabao 3-2 kwenye michuano ya Afcon iliyofanyika Misri.

DAR ES SALAAM, Tanzania -Kocha wa timu ya taifa ya Tanzania Bara, Kilimanjaro Stars, Etienne Ndayiragije amewataja wachezaji Juma Abdul wa Yanga mlinda lango wa Simba kwenye kikosi chake cha wachezaji 32 ambao anatarajia kwenda nao Uganda kwenye michuano ya CECAFA inayotarajia kuanza Desemba 7, mwaka huu.

Mbali na wachezaji hao lakini baadhi ya wachezaji wengine wapya kwenye kikosi hicho ni Lucas Kikoti (Namungo), Yusuph Mhilu (Kagera Sugar) na Paul Nonga (Lipuli). Pia jina la kinda Kelvin John lipo kwenye orodha hiyo.

Kikosi hicho kinatarajia kuingia kambini mapema kabisa wikiendi hii na kuna uwezekano mkubwa baadhi ya wachezaji wakachujwa kwenye kikosi cha mwisho ambacho kitaondoka nchini mapema wiki ijayo.

Jina la kiungo Jonas Mkude pia limo baada ya kukosekana kwenye michezo miwili iliyopita kutokana na matatizo ya kifamilia lakini hata hivyo mlinzi Erasto Nyoni hajatajwa baada pengine kutokana majeruhi aliyopata wakati wa mchezo dhidi ya Equatoria Guinea.

Juma Abdul alikuwa ni mchezaji wa timu ya taifa lakini tatizo la majeruhi lilimfanya kukosekana kwenye kikosi hicho kwa takribani miaka mitatu iliyopita.

Hata hivyo msimu huu amerejea kwa kasi kwenye kikosi cha Yanga akicheza michezo minne kati ya sita ambayo wamecheza msimu huu na akiwa sehemu muhimu ya kupatika kwa ushindi kwenye michezo yote ambayo amecheza.

Naye Manula ambaye alikuwa ni "Tanzania One" kabla ya ujio wa Ndayiragije alijikuta akipoteza nafasi yake kwa mlinda lango mkongwe Juma Kaseja ambaye amecheza mechi zote nane zilizopita.

Manula amecheza kwenye asilimia kubwa ya michezo ya Simba msimu huu lakini hakuwa chaguo la kocha Ndayiragije tangu ajiunge na Stars kuchukuwa nafasi ya Emmanuel Amunike.

Mechi ya mwisho kwa Manula kucheza akiwa na timu ya taifa ilikuwa ni mwezi Julai ambapo Stars walifungwa na Kenya kwa mabao 3-2 kwenye michuano ya Afcon iliyofanyika Misri.

Kilimanjaro Stars wapo kwenye kundi C la michuano ya CECAFA wakiwa sambamba na timu za Zanzibar, Djibouti na Kenya.

Michuano hiyo kwa mara ya mwisho ilifanyika mwaka 2017 ambapo wenjeji Kenya walifanikiwa kutwaa taji hilo kwa kuwafunga Zanzibar kwa mabao 2-1 kwenye mchezo wa fainali. 

Kikosi Kamili

Juma Kaseja (KMC), Aishi Manula (Simba), David Kisu (Gor Mahia), Metacha Mnata (Yanga), Salum Kimenya (TZ Prison), Juma Abdul (Yanga), Nickson Kibabage (Difaa El Jadid), Gadiel Michael (Simba), Mwaita Gereza (Kagera Sugar), Mohamed Hussein (Simba), Bakari Mwamnyeto (Coastal Union), Kelvin Yondani (Yanga) Abdulmajid Mangalo (Biashara United), Baraka Majogoro (Polisi Tanzania), Jonas Mkude (Simba) na Fred Tangalu (Lipuli).

Wengine ni: Zawadi Mauya (Kagera), Idd Seleman (Azam), Kelvin John (Footbal House), Mzamiru Yassin (Simba), Hassan Dilunga (Simba), Ditram Nchimbi (Polisi Tanzania), Mkandala Cleofas (TZ Prison), Paul Nonga (Lipuli), Jafar Kibaya (Mtibwa), Salum Abuubakar (Azam), Eliud Amokile (TP Mazembe), Miraji Athuman (Simba), Yusuph Mhilu (Kagera),  Eliuter Mpepo (Buildon), Shaban Chilunda (Azam) na Lucas Kikoti (Namungo).

Imeandaliwa na Badrudin Yahaya